Wednesday, May 12, 2010

NAFASI YA KUFANYA MABADILIKO 2010

Ndugu zangu watanzania,
Mbele yetu ipo nafasi ya kufanya maamuzi nyeti juu ya mustakabari wa taifa letu na juu ya mustakabari wa kila raia wa taifa hili. Tunayo nafasi nyingine mwaka huu, ya kuuondoa katika atamu mfumo ambao umeiharibu nchi kwa kuendelea kuwanufaisha watu kadhaa wachache na kuwaacha mamilioni ya watanzania katika dhiki zisizomithirika. Tunayo nafasi sasa ya kumaua kwamba taifa letu linaweza kuwa na uchumi imara kabisa na hivyo kutufanya tuondoke katika aibu ya umaskini ambayo tumedumu nayo kwa miaka mingi.
Fursa iko mbele yetu ya kuamua kwamba zile adha za kupata huduma mbovu za afya katika mahospitali yetu, elimu duni katika mashule yetu, miundombinu hafifu katika nchi yetu, sasa mwisho wake umewadia.

Kwa zaidi ya miongo minne, tumekuwa na utawala ulio mwapesi kutulaghai kwa kutuahidi kwamba utatupatia maisha bora kila mmoja wetu, kwamba unafanya jitihada za kuondoa kero za wananchi. Sote ni mashahidi kwamba ahadi zao zimegeuka kuwa uongo ama kwa sababu tokea awali walikusudia kutudanganya ili wajinufaishe wenyewe, au uwezo wao wa kushughulikia masuala haya ama kwa hakika ni mdogo.
Tunayo mamlaka ya kumwambia mwongo ya kwamba uongo wake sasa basi. Mbele yetu ni fursa ya kuthibitisha kwa vitendo kwamba hatuko tayari tena kumpa nafasi nyingine mtu yeyote aliyeshindwa kuishi maneno yake.

Kwa uamuzi tutakaoufanya mwezi Oktoba, tunaweza kabisa kuifanyia mabadiliko makubwa sana nchi yetu ili kuleta tija katika kila sekta na hatimaye tuwe na taifa lenye nguvu za kiuchumi na maendeleo ya haja.
Hata lini tutalia kwamba katika hospitali zetu wagonjwa wanalala ‘mzungu wa nne’ na hakuna dawa. Asiyetaka kusikiliza kilio hiki tunamfahamu tayari.
Hata lini tutalalamika kwamba elimu imekuwa duni, shule hazina walimu, na tuna mitaala isiyoridhisha. waliotufikisha hapo mbona tunawajua kwa majina.
Hata lini tutanungumika kwamba mwananchi wa kawaida hafaidishwi na uchumi wan chi, bali wageni na wenye nacho tayari. Aliyecheza hii kamali mbona tunamfahamu.
Hata lini tutastaajabia kuona watawala wakiishi kwa anasa na starehe ilihali wananchi wakitaabika katika dhiki. Waliojenga utaratibu huu, na wasikuwa tayari kuona unabadilika tunawamanya.
Ni nani basi awe ‘Yuda’ wa taifa letu kwa mwaka huu hata aendelee kutumia kura yake kuwapa mafisadi hatamu za utawala? Tafadhali, sio wewe msomaji.
Ni nani basi awe mzalendo wa kweli kwa taifa letu hata atumie upigaji kura wake kulibadilisha Taifa. Naam, unao uamuzi, jiunge na wenye nia hiyo.

0 comments: